Post Details

CHUO CHA UONGOZI WA MAHAKAMA LUSHOTO CHAPITIA MTAALA WAKE

Published By:faustine.kapama

Na Seth Kazimoto-Mahakama Kuu, Arusha

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa kushirikiana na wadau, kimeanza kikao kazi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Arusha kupitia mtaala wake ili kuendana na hali halisi ya soko la sasa la ajira na mabadiliko ya kiteknolojia na uchumi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho hivi karibuni, Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama wa IJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda alieleza kuwa mapitio ya mtaala wanayofanya yanahusisha uingizaji wa Mwongozo wa Utoaji Adhabu (Sentencing Guidelines) ili kuuboresha na hatimae Chuo kuweza kutoa wahitimu mahiri katika taaluma wanazosoma.

Alisema katika kikao kazi hicho kitakachohitimishwa tarehe 22 Septemba, 2023 kuwa kufanyika kwa mapitio ya mtaala wa Chuo hicho kunatarajiwa kuleta mafanikio makubwa hasa katika kukidhi mahitaji ya soko la ajira.

“Wanachuo watakaokuwa wanahitimu katika Chuo watakuwa na uelewa wa kina na uwezo mkubwa wa kufanya kazi walizosomea. Chuo kitaongeza wigo wa mafunzo yake na hivyo kukuza ushirikiano na waajiri pamoja na wadau, na hatimae kusaidia katika kukuza uchumi wa nchi,” Mhe. Dkt. Kisinda alisema.

Alibainisha pia kuwa Mahakama itanufaika kwa kuajiri wahitimu kutoka IJA wenye weledi wa kazi na hivyo kuiwezesha kutimiza majukumu yake ipasavyo na kupelekea uwepo wa taswira chanya ya wananchi kwa Mhimili huo.

Mkurugenzi huyo alisema imani kubwa ya wananchi kwa Mahakama itawafanya kupeleka migogoro yao mahakamani na kuwezesha utawala wa sheria kustawi nchini.

Wajumbe mbalimbali wanahudhuria kikao Kazi hicho, wakiwemo Makamu Mkuu wa Chuo-Taaluma, Tafiti, na Ushauri Elekezi, Bw. Goodluck Chuwa, Mkufunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma-Magogoni Dar es Salaam, Bi. Khadija Ramadhani, Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala -Mahakama ya Tanzania, Bw. Stephen Magoha na Mkurugenzi wa Kumbukumbu na Nyaraka wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula.

Kikao kazi hicho kimefadhiliwa na programu ya kujenga mfumo endelevu wa mapambano dhidi ya rushwa nchini, yaani Building Sustainable Anti-Corruption Action in Tanzania (BSAAT).

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Comments (0)

Leave a Comment