Post Details

KUNDI LA KUMI LAANZA MAFUNZO YA UDALALI NA USAMBAZAJI NYARAKA ZA MAHAKAMA

Published By:kansha.innocent

  •         Washiriki kujengewa weledi na umahiri katika eneo hilo
  •         Watakaofaulu kupata cheti cha kuwawezesha kuomba kazi hiyo

Na. Innocent Kansha - Mahakama

Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Bw. Goodluck Chuwa leo tarehe 20 Machi, 2023 amefungua mafunzo kwa watu 27 wenye nia ya kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka za Mahakama, washiriki wa mafunzo hayo ni kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania.

Akifungua mafunzo hayo ya kundi la 10 toka kuanzishwa kwake yanayofanyika katika Taasisi ya Mafunzo ya Sheria kwa Vitendo jijini Dar es Salaam, yanayoendeshwa na IJA kwa muda wa wiki mbili. Bw. Chuwa amesema, mafunzo yanayotolewa ni sehemu ya maboresho ya Mahakama yenye lengo la kujenga weledi na umahiri kwa wadau hao na hivyo kupunguza malalamiko na kujenga taswira nzuri ya Mahakama mbele ya umma.

“Msingi na msukumo wa uendeshaji wa mafunzo haya unatokana na malalamiko ya wadau wa Mahakama yanayoelekezwa moja kwa moja kwa madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama dhidi ya ukosefu wa maadili na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao”, alisema Chuwa

Aidha, Bw. Chuwa alisema, washiriki watakapomaliza mafunzo hayo na kuhitimu kisha kusajiliwa na Mahakama kutekeleza majukumu ya udalali na usambazaji nyaraka za Mahakama wataisaidia Mahakama kutenda haki kwani nafasi hizo watakazozitumikia zitaongeza imani ya wananchi kwa Mahakama.

“Niwasihi kuwa baada ya kupata mafunzo haya, kufuzu mitihani yenu mkafanye kazi mkitanguliza uadilifu kwa kuzingatia kanuni na maadili mliyofundishwa ili kukidhi kiu ya Mahakama ya kuwahudumia wananchi kwa kutoa haki kupitia wadau wengine ikiwemo madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama”, Chuwa alisisitiza.

Akifafanua moja ya malengo ya kuazisha progamu hiyo, mgeni rasmi huyo alisema, kuanzishwa kwa mafunzo ni mojawapo ya zao la maboresho makubwa yanayoendelea katika mhimili wa Mahakama wenye lengo la kuondoa malalamiko mengi yaliyokuwepo kutoka kwa wananchi na moja ya eneo lenye kulalamikiwa ni ukosefu wa uadilifu wakati wa utekelezaji wa majukumu ya udalali na usambazaji wa nyaraka za Mahakama, kwa kufanya hivyo kutawawezesha Madalali na Wasambaza nyaraka za Mahakama kufanya kazi kwa uadilifu na kufuata kanuni zilizopo.

Bw. Chuwa aliongeza kuwa, ni vizuri kutambua kuwa uamuzi wa kuanzisha mafunzo hayo ya wenye nia ya kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka za Mahakama ni kutokana na changamoto ya muda mrefu ya  upatikanaji wa Madalali na Wasambaza nyaraka za Mahakama wenye sifa na hivyo Mahakama kupitia Mpango Mkakati wake wa kwanza wa mwaka 2015/2016 – 2019/2020 na Mradi wa Uboreshaji wa Mahakama kupitia mradi wa huduma zinazomlenga mwananchi, iliandaa kanuni ziitwazo Kanuni za Uteuzi, Gharama, Malipo na Nidhamu za Madalali na Wasambaza Nyaraka za Mahakama kwa Tangazo la Serikali Namba 363 la 2017 (The Court Brokers and Process Servers (Appointment, Remuneration and Disciplinary) Rules, GN. 363 of 2017).

Kanuni hizo zilitoa maelekezo kwamba, madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama wanapaswa kusoma kozi za muda mfupi ambazo itawapa weledi katika kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka kwa ufanisi.

Chuwa alifafanuwa kwa washiriki hao kuwa, watajifunza mambo mengi sana katika kipindi hicho cha wiki mbili, yakiwemo masuala ya muundo wa Mahakama ya Tanzania, utaratibu wa mashauri ya madai, usambazaji wa nyaraka za mahakama, utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama na maadili ya madalali na wasambaza nyaraka za mahakama na nyinginezo.

“Ninawasihi watumieni wawezeshaji wenu ambao ni Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Naibu Wasajili na Mahakimu ambao  ni wabobevu, wazoefu na mahiri katika eneo la sheria na taratibu za udalali na usambaza nyaraka za Mahakama kuibua mijadala huru itakayowasaidia kuongeza ujuzi na Msisite kuchangia uzoefu wenu kwa lengo la kuongezeana maarifa”, Chuwa aliwashauri washiriki hao

Washiriki hao, watafundishwa na wataalamu wabobezi na mwisho wa siku watapewa mtihani na wale tu watakaofaulu ndiyo watapewa cheti kitakachowawezesha kuomba kazi hiyo Mahakama Kuu ya Tanzania.

Kutokana na msingi huo, kundi hili la watu wenye nia ya kufanaya kazi ya udalali na usambazaji wa nyaraka za Mahakama ni la kumi (10) tangia mafunzo ya namna hiyo yazinduliwe na hadi kufikia sasa jumla ya washiriki 262 wamedahiliwa kwa mafunzo hayo na washiriki 141 wamefaulu na kufuzu kigezo cha kuomba kazi ya udalali na au usambaza nyaraka za Mahakama.

Comments (0)

Leave a Comment