Published By: | faustine.kapama |
---|
Na. Eva Leshange-Mahakama, Singida
Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida na Mahakama ya Wilaya Singida jana tarehe 9 Machi, 2023 zilikutana na wadau katika kikao cha kusukuma mashauri ya jinai na madai kujadili namna ya kuondokana na mlundikano
Kikao hicho ambayo kiliongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa kilihudhuliwa na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Manyoni na Iramba, wakuu wa taasisi za Serikali katika Mkoa, ikiwemo TAKUKURU, Magereza, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Mkuu wa Upelelezi na Mganga Mkuu.
Kwenye kikao hicho, wadau hao walisisitiza kasi ya umalizaji wa mashauri iendane na kesi zinazofunguliwa ili kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati. Kikao hicho pia kimeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha mashauri ya mlundikano yanapungua katika ngazi zote za Mahakama na kuzuia kuwepo mahakamani.
Baadhi ya mikakati iliyowekwa ni pamoja na kutoahirisha mashauri kwa muda mrefu, usuluhishi upewe kipaumbele na wadau kuelimishwa, Video Conference itumike ipasavyo hasa kwa mashahidi wa mbali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka iongeze kasi ya kutoa vibali kwa mashauri yanayohitaji kibali hicho kabla ya kusikilizwa.
Mikakati mingine ni kutekeleza ipasavyo muongozo wa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) katika usikilizaji wa mashauri kwa kuzingatia muda ulioelezwa wa kusikiliza mashauri na kuwa na “clean up session” kila baada ya miezi ya mitatu kwa kutenga mwezi mmoja wa kusililiza mfululizo mashauli yote yaliyopo katika mlundikano na yale yanayo karibia.
Aidha, waendesha mashtaka wameomba kuwe na mawasiliano baina yao, mawakili wa kujitegemea na Mahakimu, hasa katika kupeana taarifa za shauri limefikia muda gani toka kufunguliwa na kuweka alama tambuzi kwa yale yote yanayo karibia kuingia kwenye mlundikano ili kuyapa kipaumbele.
Kadhalika madaktari wamekumbushwa kujaza fomu za PF3 kwa wakati sio hadi mgonjwa apone ili kuepuka jalada kukaa katika hali ya upelelezi kwa muda mrefu.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro)