Post Details

IJA NA CHUO CHA DIPLOMASIA KUSHIRIKIANA KATIKA ENEO LA ITIFAKI NA ADABU.

Published By:kansha.innocent

Na. Innocent Kansha-Mahakama

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kimeingia makubaliano ya ushirikiano na Chuo cha Diplomasia “Centre for Foreign Relation” wenye lengo kuwajengea uwezo uwezo watumishi wa Mahakama kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo eneo la itifaki na adabu “Protocal and Etiquette”

Makubaliano hayo yamesainiwa leo tarehe 22 Mei, 2023 Mahakama ya Rufani ya Tanzania jijini Dar es salaam kati ya Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Faustin Kihwelo pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Chuo cha Diplomasia Kurasini, Bw. Felix Wandwe.

“Makubaliano hayo yanalenga kujengeana uwezo katika nyanja mbalimbali ikiwemo utafiti, ushauri wa kitaalamu na uandaaji wa mafunzo, mikutano, warsha na makongamano”, alisema Jaji Dkt. Kihwelo

Jaji Dkt. Kihwelo aliongeza kuwa makubalianao hayo yamefanyika wakati muafaka ili kukuza uelewa na weledi wa namna bora ya kuratibu na shughuli/hafla mbalimbali za kimahakama na Chuo.

“Mfano katika Taasisi kama Mahakama, Maafisa wengi hupendelea kuvalia tai yenye rangi nyekundu lakini ukifuata misingi ya itifaki na adabu tai nyekundu inapaswa kuvaliwa na Mkuu wa Mhimili yaani Jaji Mkuu wa Tanzania, jambo hili limekuwa likitolewa elimu mara kwa mara kuepusha kuharibu itifaki” alisema Jaji Dkt. Kihwelo.

Jaji Dkt. Kihwelo aliongeza kuwa tayari Chuo kimeandaa andiko maalumu la kuratibu shughuli zote zinazohusu itifaki na adabu na litawasilishwa Chuo cha Diplomasi ili kushirikishana kwa lengo la kuboresha zaidi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Chuo cha Diplomasia Bw. Felix Wandwe hakusita kutoa shukrani zake kwa kusaini makubaliano na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) katika mashirikiano ya kuboresha ujuzi katika eneo la itifaki na adabu.

“Binafsi nimekitembelea Chuo cha IJA na nimeona kuna mambo mengi sana tuayoweza kufanya kazi pamoja kama vile masuala ya upatanishi na usuluhishi, mbinu za majadiliano (negotiations skills) tuna Walimu wabobevu pale Chuo cha Diplomasia na hasa ndiyo maeneo tuliojikita kutoa elimu zaidi ya masuala ya itifaki na adabu”, alisema Mkurugezi huyo.

Bw. Wandwe aliongeza kuwa, kuna mambo mengi yanayofanywa na Chuo cha Diplomasia yanayoingiliana moja kwa moja na shughuli za kimahakama za utatuzi wa migogoro, ushauri kwa viongozi na kuwaongezea weledi katika mbinu za kutatua migogoro.

Bw. Wandwe alisema, katika utekelezaji wa makubaliano hayo utaandaliwa Mpango Kazi utakaosaidia kutekeleza majukumu yaliyoainisha ndani ya makubaliano hayo, kwa maana ya kuonyesha muda maalumu wa utekelezaji wa kila shughuli iliyoanishwa.

“Uzoefu unaonyesha kuwa makubaliano mengi yanayoingiwa kati ya taasisi nyingi yamekuwa hayatekelezi kwa sababu ya kutokuwa na muda maalumu wa utekelezaji wa majukumu yaliyoanishwa kufanyiwa kazi, hili letu litafanyika kwa nguvu zote kulifanikisha”, aliongeza Mkurugenzi huyo.

Comments (0)

Leave a Comment