Post Details

JAJI MKUU AWATAKA MAHAKIMU KUJIANDAA KUSIKILIZA MASHAURI YA ARDHI

Published By:LYDIA CHURI

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mahakimu kuwa   na utayari wa kuanza kusikiliza mashauri yanayohusu ardhi ili kutatua changamoto na malalamiko yaliyojitokeza kwenye eneo hilo kupitia Mabaraza ya Ardhi, hali iliyosababisha mabaraza hayo kwenda Serikalini.

Akizungumza leo mara baada ya kumuapisha Hakimu Mkazi, Mhe. Olivia Towilo ofisini kwake, iliyopo Mahakama ya Rufani Tanzania, Jijini Dar es Salaam, Jaji Mkuu alisema Mahakama imekuwa ikifanya vizuri ndiyo maana Serikali imeona ikabidhi jukumu hilo katika mhimili huo.

“Kuanzia mwaka wa fedha ujao yaani 2020/2021 Mahakama itaanza kusikiliza mashauri ya ardhi, hivyo tumeongezewa mzigo Mahakimu watapewa mashauri. eneo hili lina mashauri mengi, changamoto na malalamiko.

“Mimi naona Mahakimu ninyi muwe mstari wa mbele kuhakikisha kwamba changamoto na malalamiko yaliyojitokeza kupitia mabaraza ya Ardhi hali iliyosababisha suala hili kwenda Serikalini yanatatuliwa,’’ alisema Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu aliongeza kwamba anatarajia Mahakama itafanya kazi hiyo kwa ubora na kutenda haki na kutoa kwa wakati, kutatua migogoro, ikiwemo kutorudia makosa yaliyojitokeza hapo awali.

Aidha Prof. Juma  aliwataka  mahakimu hao, kuwa mstari wa mbele wa utoaji wa haki  kwa kuwa hivi sasa kutokana na janga la ugonjwa wa homa ya mapafu (COVID 19) unaosababishwa na virusi vya Corona utendaji kazi wa Mahakama umebadilika kwa kutumia Teknolojia  ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

“Mahakimu sasa wako mstari wa mbele  katika mapambano hayo wanapofanya kazi ya  utoaji haki, hivyo wana changamoto ya  kuangalia afya zao na watu wanaofika mahakamani ili kuepusha kuenea kwa virusi vya Corona,’’ alisisitiza huku akisema kazi ya uhakimu ni muhimu kwa kuwa asilimia 80 ya mashauri yote yanayosajiliwa na yanasikilizwa katika Mahakama za Mahakimu.

Pia alifafanua kuwa unapozungumzia haki kwa mwananchi wa kawaida anatambua kuwa ni Hakimu, ambapo aliwataka Mahakimu hao  kutoa haki kulingana na viapo vyao.

Aliongeza kuwa Mahakimu wanapaswa kutumia elimu waliyonayo kujiendeleza kutafuta taarifa mbalimbali bila hata ya kupata cheti kwani katika karne ya 21 ya us ushindani na TEHAMA, hivyo wanatakiwa kuwa weledi katika suala hilo, uandishi na lugha ili hukumu zao ziwe zinasomeka na kueleweka.

Hakimu huyo aliyeapishwa ametokea katika Mahakama ya Mwanzo Arusha Mjini (Maromboso).

 

Comments (1)

  • Photo Loading... Edwin maiga

    Mimi ningeomba MH. Jaji mkuu aruhusu kuajili watu wenye degree na diploma za sheria katika mabaraza ya aridhi ili hata Kama haki itatokea kukwepwa Basi kuwe na sheria inayoipatia mahakama za Tz kumsikiliza mashauri hayo. LAKINI pia nishauri TU KUWA Ni vyema Kama wakiruhusu watu wa diploma na degree za sheria kusikiliza mashauri Basi mahakama za mwanzo zingekuwa mahakama za rufaaa ili Sasa mahakimu wajikite katika utaalamu uliotokana na shule ya sheria kwa vitendo.

    27-05-2020

Leave a Comment