Post Details

MAHAKAMA YAENDELEA KUWEKA MIKAKATI YA KUKABILIANA NA CORONA

Published By:LYDIA CHURI

Na Magreth Kinabo- Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi amewakumbusha wapelelezi na waendesha mashtaka  kuhakikisha kesi za jinai zinakamilishwa upelelezi wake kabla ya kufunguliwa mahakamani.

Aidha Jaji Kiongozi ameziagiza Mahakama za Hakimu Mkazi pamoja na Mahakama za Wilaya kuhakikisha  kwamba  kesi zinazofunguliwa  zinazingatia matakwa  ya Tangazo la Serikali  Na. 296 la mwaka  2012  linalotoa mwongozo wa kesi nyingi isipokuwa zile  zinazohusisha makosa makubwa kufunguliwa baada ya kukamilishwa kwa upelelezi  ili kuepusha kuongeza mlundikano usio wa lazima magerezani.

Akizungumza na waandishi wa habari leo kwenye Kituo cha Mikutano  ya waandishi wa habari cha Mahakama ya Tanzania(JMC), Dkt. Feleshi amesema kuwa kesi zote za Mahakama za Mwanzo zifunguliwe baada ya mlalamikaji kuwa ameshandaa mashahidi wake na Mahakama kujiridhisha mshtakiwa yupo na apewe fursa ya kuita wadhamini.

Alisema kwamba Mahakama imechukua hatua hiyo ili kuepuka msongamano wa mahabusu na wafungwa mahakamani,  ikiwa ni jitihada ya hatua ya kuweza kukabiliana na maambukizi  ya Virusi vya COVID 19 vinavyosababisha   ugonjwa wa Corona vilivyosambaa nchi nyingi duniani.

Dkt. Feleshi alisema kutokana na matumizi ya Tehama, hivi sasa watuhumiwa waliopo katika magereza ya Keko na Segerea hawatalazimika kufikishwa mahakamani.

‘‘Mahakama itaongeza matumizi ya Mahakama inayotembea (Mobile Court) kwa kadri mahitaji yanapotokea, pia inaendelea kujipanga zaidi juu ya hatua zingine za uwezeshaji wa usikilizaji wa mashauri na upatikanaji wa huduma nyingine za kimahakama,’’ alisema Jaji Kiongozi.

Alifafanua kuwa Mahakama itahakikisha mashauri yanasajiliwa kwa njia ya  kielektroniki yanahudumiwa mara tu yapofika kwenye mfumo na taarifa zimrudie mteja ndani ya muda mfupi. Aliongeza kuwa Mahakama kupitia Kurugenzi yake ya Usimamizi wa  Mashauri na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano

(TEHAMA) inaandaa timu ya itakayotoa msaada na ushauri wa  kiufundi kwa saa 24.

‘Mahakama itaendelea na mfululizo wa programu ya elimu ya namna ya kusajili mashauri, kupata  taarifa pamoja na kutoa msaada wa usajili wa mashauri kwa njia ya kielektroniki kwa kuanza na Mahakama zenye mashauri mengi, ambazo zinaweza kusababaisha mkusanyiko wa watu wengi,’’ alisisitiza.

Alisema chini ya  usimamamizi wa waheshimiwa  Majaji Wafawidhi  Mahakama   kwa kufuata sheria na miongozo iliyopo, zitakuwa zikitoa ratiba za usikilizaji wa mashauri hayo kwa muda maalumu. Hivyo wadaawa wanashauriwa kuwa makini na kuzingatia muda wanaopangiwa kufika mahakamani na kuhakikisha namba zao za mawasiliano ziko kwenye fomu ya kufungulia kesi au hati za kesi.

Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Lameck Mlacha aliwataka wadaawa na mashahidi kutoa ushirikiano na kuhakikisha wananawa mikono wanapofika kwenye mahakamani.

Aliongeza kwamba idadi ya watu wanaofika mahakamani ili kumwona Hakimu inapaswa kupungua na kubaki wadaawa na mawakili tu.

Akizungumzia mashauri, Jaji Mfawidhi huyo alisema Mahakama za  Wilaya za Kinondoni na Ilala nazo zitawekewa mfumo wa TEHAMA ili  ziweze kuendesha  mashauri kwa mtandao.

Alitoa wito kwa watumishi wa Mahakama, waadawa pamoja na wananchi kushirikiana kwa pamoja katika kuwezesha matumizi ya TEHAMA ili kuendeleza mapambano ya kujikinga na ugonjwa huo na haki kupatikana kwa wakati.

 

 

Comments (0)

Leave a Comment