Post Details

RAIS MAGUFULI KUZINDUA JENGO LA MAHAKAMA YA WILAYA CHATO

Published By:LYDIA CHURI

Na Lydia Churi- Chato, Geita

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kesho anatarajiwa kuzindua jengo jipya la Mahakama ya wilaya ya Chato ambapo wilaya hiyo pamoja na baadhi ya wilaya na Mikoa nchini hivi sasa ina majengo ya kisasa yanayorahisisha utoaji wa huduma za Mahakama.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mkoani Geita, Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Robert Gabriel amesema majengo mengine mawili mapya ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita na Mahakama ya wilaya ya Bukombe yatazinduliwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma Alhamis Desemba 19 mwaka huu.

Kuzinduliwa kwa jengo la Mahakama ya wilaya ya Chato kutaongeza idadi ya Wilaya na Mikoa yenye majengo mapya na ya kisasa ya Mahakama. Wilaya zenye majengo mapya ni pamoja na Ruangwa, Mkuranga, Kigamboni, Ilala, Bagamoyo, Kondoa, Longido, Kilwa na Bukombe. Baadhi ya mikoa yenye majengo mapya ni Pwani, Simiyu, na Geita. Mahakama ya Tanzania inaendelea na ujenzi wa majengo yake katika maeneo mbalimbali nchini.

Mkuu wa Mkoa wa Geita amesema, sambamba na uzinduzi wa majengo ya Mahakama, Rais Magufuli pia ataweka jiwe la msingi ujenzi wa jengo la ofisi ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wilayani Chato.

Aidha, Rais Magufuli pia ataweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Msikiti wa kisasa (Al-Huda) pamoja na kuzindua miradi ya visima vya maji katika maeneo ya shule ya msingi Chato pamoja na kuzungumza na wananchi wa mkoa wa Geita na Taifa kwa ujumla.  

Mkuu huyo wa Mkoa pia alitoa wito kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri kuwawahisha wananchi kwenye matukio haya muhimu kwa maendeleo ya taifa pamoja na wananchi kwa ujumla.

Comments (0)

Leave a Comment