Na ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro.
Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam hivi karibuni walifanya ziara ya utalii wa ndani kwa kutembelea Mbuga ya Wanyama Mikumi pamoja na kupanda milima ya Uluguru mkoani hapa.
Ziara hiyo iliyoongozwa na Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi, Mhe. Franck Kiswaga na Mtendaji, Bi. Athanasia Kabuyanja, ilikuwa sehemu ya kujifunza kuhusu haki na ustawi wa wanyama pamoja na kuimarisha afya kupitia mazoezi ya kupanda milima.
Kadhalika, ziara hiyo ilifanyika kwa lengo la kuhamasisha utalii wa ndani, kuongeza uelewa wa watumishi kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira na viumbe hai, sambamba na kukuza mshikamano miongoni mwao.
Aidha, ziara hiyo iliwapa fursa ya kujifunza kwa karibu kuhusu haki za wanyama, sheria zinazowalinda na wajibu wa kila mmoja katika kulinda bioanuai ya Taifa. Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, mmoja wa watumishi alisema:
"Tumepata kujifunza jinsi wanyama wanavyolindwa kisheria na changamoto wanazokutana nazo. Hii ni elimu muhimu kwa watumishi wa Mahakama kwa kuwa tuna wajibu wa kuhakikisha haki inatendeka kwa viumbe vyote."
Wakiwa katika mbuga hiyo, watumeshi hao wa Mahakama walifanikiwa kuwaona Wanyama mbalimbali, wakiwemo Swala, Pundamilia, Tembo, Twiga na wengine wengi.
Kupitia kupanda milima ya Uluguru, watumishi hao walijijengea afya, kuimarisha ushirikiano na kuondoa msongo wa mawazo, hatua ambayo inasaidia kuongeza ufanisi kazini.
Ziara kama hiyo imeelezwa kuwa chachu ya kuhamasisha watumishi wa umma kuthamini vivutio vya ndani na kuchangia maendeleo ya sekta ya utalii nchini.